SERIKALI KUFUTA MISAMAHA YA KODI YA VAT NCHINI
Serikali
itawasilisha Bungeni rasimu ya maboresho ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT)
ambayo itafuta misamaha ya kodi hiyo.
Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema jana
kwamba mpango huo unafanyiwa uchambuzi na Serikali na kwamba utawasilishwa
katika Bunge la Bajeti wiki mbili zijazo.
Kwa nyakati
tofauti, mwenyekiti wa CUF ambaye pia ni mtaalamu wa uchumi, Profesa Ibrahim
Lipumba alikuwa akipigia kelele juu ya wingi wa misamaha ya kodi akisema
imekuwa ikipoteza kiasi kikubwa cha mapato ya Serikali.
Profesa Lipumba
alisema hivi karibuni kuwa ili kuondoa kasi ya ukuaji wa nakisi, Serikali
inatakiwa kufuta kabisa misamaha holela ya kodi inayofikia Sh1.8 trilioni
ambayo ni sawa na asilimia tano ya pato la taifa.
Siku tano
zilizopita, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, wakati akiwasilisha mpango wa Bajeti
ya mwaka 2014/15 kwa wabunge, alisema Serikali imepanga kukamilisha utungwaji
mpya wa Sheria ya VAT.
Alisema hatua hiyo
itakwenda sambamba na kuongeza wigo wa kodi kwa kuimarisha vyanzo vilivyopo na
kuanzisha vyanzo vipya pamoja na kurasimisha sekta isiyo rasmi ili iingie
kwenye mfumo rasmi wa kodi.
Katika bajeti ya
mwaka 2013/14, Serikali iliondoa msamaha wa VAT kwa viwanda vya nguo
vinavyotumia pamba ya ndani.
Kwa mujibu wa
ripoti ya utafiti ya taasisi ya CRC Sogema ambayo inaishauri Wizara ya Fedha,
misamaha chini ya Kodi ya VAT ilifikia Sh802 bilioni kwa mwaka 2012, wakati
jumla ya misamaha yote ilikuwa Sh1.8 trilioni.
Ripoti hiyo ya
mwaka 2013 inasema: “Matokeo ya utafiti huu muhimu yanapendekeza kuwa kuna
ufanisi zaidi kwa nchi zinazoendelea kujikita zaidi katika kuweka mazingira
mazuri ya uwekezaji kuliko kutoa misamaha ya kodi kwa mashirika.”
Jana, Lukuvi
alisema: “Serikali ina mpango huo na hivi sasa rasimu ya VAT bado inaandaliwa
na jambo hilo lipo mikononi mwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.”
![]() |
Waziri wa Nchi, Ofisi ys Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi |
No comments:
Post a Comment